MAMLAKA ya Bandari Tanzania (TPA) imesema kuwa baadhi ya vifaa vitakavyotumika katika mradi wa ujenzi wa gati maalumu la magari na uboreshaji wa gati namba 1 -7, vimewasili jijini Dar es Salaam tayari kwa kuanza ujenzi katikati ya Novemba mwaka huu.
Meneja wa Bandari ya Dar es Salaam, Fredy Liundi alisema jana alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu kuwasili kwa vifaa hivyo na kuanza kwa ujenzi huo wa mradi ujulikanao kama ‘Dar es Salaam Maritime Gateway Project’.
Liundi alitaja vifaa vilivyowasili kuwa ni meli tano, tatu kati ya hizo zimeleta vifaa vya ujenzi na mbili zitatumika kuchimba kwa lengo la kuongeza kina cha bandari.
Alisema mradi huo utakapokamilika utaongeza uwezo wa Bandari ya Dar es Salaam kuhudumia meli kubwa kutoka urefu wa meta 243 za sasa zenye uwezo wa kubeba makontena kati ya 2,500 na 4,000 hadi kufikia meli zenye urefu wa meta 320 na uwezo wa kubeba makontena kati ya 6,000 hadi 8,000.
Vile vile utaongeza uwezo wa kuhudumia shehena za mizigo kutoka tani milioni 15 za sasa hadi kufikia tani milioni 28 ifikapo mwaka 2022.


Post A Comment: