Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe amesema gharama za matibabu ya Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu aliyelazwa katika Hospitali ya Nairobi nchini Kenya zimefikia Sh412.7 milioni.
Lissu ambaye ni mwanasheria wa chama hicho, amelazwa hospitalini hapo tangu Septemba 7 aliposhambuliwa na kujeruhiwa kwa risasi akiwa maeneo ya nyumbani kwake Area D mjini Dodoma.
Mbowe akizungumza na waandishi wa habari jana Jumanne, Oktoba 17, 2017 jijini Dar es Salaam, Tanzania amesema gharama ni kubwa, ila anawaomba Watanzania wasichoke kuchangia kwa kuwa Lissu atarudi barabarani.
“Tunaishukuru sana familia ya Lissu, imekuwa na msimamo kama Lissu mwenyewe. Tumefanya kazi na familia na tutaendelea kufanya kazi na familia. Tutakapokwenda katika matibabu ya tatu, tutaiacha kwa familia iwe msemaji wa kwanza, mgonjwa anaweza kuongea na kujitambua,” amesema.



Post A Comment: