ads

Baadhi ya wawekezaji kutoka China wamesema kupanda kwa gharama za maisha, hali ngumu ya uchumi na makato makubwa ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) kumewasababishia hasara iliyowafanya baadhi yao kukimbilia nchi za jirani na wengine kurejea kwao.


Wawekezaji hao walikuwa wakizungumza wakati wa ziara ya timu ya waandishi wa habari wa China na Tanzania yenye lengo la kufungua pazia la ushirikiano wa vyombo vya habari baina ya nchi hizo mbili katika kuandika na kutangaza taarifa za uwekezaji zinazofanywa na nchi hizo.

Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya Sunshine Group, Tonny Sun alisema tozo ya asilimia 18 ya VAT ni kubwa hasa kipindi hiki ambacho biashara nyingi zimeyumba.

Sun alisema ikiwa hali ya biashara itaendelea kama ilivyo, inahatarisha uwekezaji japo kampuni yake iliyotumia zaidi ya dola 100 milioni (Sh216 bilioni) kuwekeza nchini  inaendelea kujitahidi ili ifikie malengo yake ya kuwasaidia wananchi.

“Hali ya biashara imekuwa ngumu sana, wenzetu wengine kama asilimia 30 ya wawekezaji wa China wameshindwa kwa sababu hali ya biashara imekuwa ngumu, wapo waliohamia nchi za jirani na wengine wamerudi nyumbani, hali ya biashara imekuwa ngumu,” alisema.

Alisema kampuni yake yenye viwanda zaidi ya vitano vikiwamo vya kuzalisha mafuta ya alizeti na korosho, imeajiri wafanyakazi wazalendo 1,600 na kwamba wakulima wanaowauzia mazao kwa ajili ya kutengeneza bidhaa zao, wananufaika na uwepo wa soko la uhakika.

Aliiomba Serikali isaidie kupunguza kodi kwenye baadhi ya bidhaa za msingi zinazochangia kuinua pato la wananchi wa chini ili kuwawekea mazingira mazuri ya kuendelea na kazi yao.

Ofisa Mtendaji Mkuu wa Star Times, Leo Liao alisema kwa sasa kampuni yake haipati faida kutokana na hali ngumu ya uchumi iliyosababisha asilimia 50 ya wateja wake kushindwa kulipia gharama za ving’amuzi kwa mwezi.

Alisema hali hiyo imewafanya wapunguze bei hadi kufikia Sh6,000 kwa mwezi lakini bado hali imekuwa ngumu.

“Hakuna faida na tunajiendesha kwa hasara kwa sababu ya hali ngumu iliyopo, ninavyoona tunaelekea kufa kabisa kibiashara kwa sababu asilimia 50 ya wateja wetu hawajaweza kulipia huduma. Tunajitahidi kuendelea kutoa huduma nzuri kwa wateja wetu, tumepunguza bei na wateja wanaweza kulipia kwa siku tano hadi wiki moja,” alisema.

Aliiomba Serikali kufuta chaneli zinazoonekana bure ikiwa mteja atashindwa kulipia gharama kwa madai kuwa jambo hilo pia linachangia watu kutolipia.

“Hali ya uchumi imekuwa ngumu na kwa sababu chaneli nyingine ni bure, basi unakuta watu hawalipii kabisa,” alisema.
DOWNLOAD APP YETU YA SWAHIBA NEWS ILI UWEZE KUPATA HABARI ZOTE MOJA KWA MOJA KUPITIA SIMU YAKO YA MKONONI BILA KUINGIA KWENYE WEBSITE,KUDOWNLOAD BONYEZA HAPA  

ANDIKA MAONI YAKO HAPO CHINI
ads
Bonyeza HAPA kudownload applicationi ya SWAHILI NEWS kwenye simu yako ili kupata habari zetu Haraka
Share To:

SWAHIBA MEDIA STAFF

Habari , karibu katika mtandao wetu ili kuhabarika na stori zote za siku katika lugha yetu adhwim ya kiswahili, habarika wakati wote weka dunia kiganjani mwako na swahili news

Post A Comment: