ads

MKULIMA aliyechomwa mkuki mdomoni na kutokea shingoni, Augustino Mtitu (35), amepata pigo lingine baada ya familia yake ya mke na watoto watano, kutoweka nyumbani na kwenda kusikojulikana.


Familia hiyo iliyokuwa ikiishi katika Kitongoji cha Upangwani Kijiji cha Dodoma Isanga Kata ya Masanze Wilaya ya Kilosa mkoani Morogoro, imetoweka katika makazi yake hayo ikihofia vitisho dhidi yao vinavyodaiwa kutolewa na baadhi ya wafugaji nyakati za usiku.

MTITU AIANGUKIA SERIKALI

Aidha, majeruhi huyo ambaye amelazwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro kwa matibabu baada ya kupataa taarifa za familia yake kuyakimbia makazi yake, ameiangukia serikali akiiomba ichukue hatua za makusudi kuhakikisha amani inapatikana katika eneo hilo.

Pamoja na familia hiyo kuondoka katika makazi yake, pia familia nyingine tisa zenye idadi ya watu kati ya watano na sita katika kitongoji hicho, nazo zimeyakimbia makazi yake na kwenda kutafuta hifadhi katika vijiji vya jirani kwa hofu kama hiyo.

Nipashe lilifika katika Kitongoji cha Upangwani kwenye nyumba anayoishi majeruhi Mtitu na kukuta si mkewe Maria Msanga wala watoto wake, Pili (16), Lavuma (14), Josephine (10), Misio (7) na Simon (3), hawapo katika makazi hayo huku nyumba yao ikiwa imetiwa kufuli.

Akizungumzia na Nipashe,baba mdogo wa mke wa Mtitu anayeishi katika kitongoji hicho pia Mwalongo Sangu, alisema familia hiyo iliondoka na kutelekeza nyumba hiyo tangu Desemba 26, mwaka huu ikidai inakwenda kutafuta sehemu nyingine ya kujihifadhi kutokana na tishio la wafugaji.

Sangu alisema familia hiyo ilipata hofu kutokana na maneno ya baadhi ya wafugaji waliokuwa wanapita katika kitongoji hicho usiku wakiwa na tochi na kuwatishia kuwa endapo wataendelea kufukuza mifugo yao katika mashamba ya wakulima, watawafanyia vitendo hivyo wengine.

"Mimi huyo Mtitu aliyechomwa Mkuki mdomoni, ni kama mwanangu pia kwa kuwa mkewe ni mtoto wa kaka yangu kabisa. Waliondoka na kukimbia nyumba, hii ni siku ya pili baada ya tukio akiwa mama na watoto wake watano na hatujui wamekwenda kutafuta hifadhi wapi. Taarifa nilionayo wamekuwa wakitishiwa na wafugaji wanaopita usiku katika kitongiji chetu," alisema Sangu.

Kwa mujibu wa Sangu, watoto watatu kati ya watano wa Mtitu (Lavumo, Josephine na Misio), wanasoma katika Shule ya Msingi Nyari iliyopo kijiji cha jirani.

Sangu alieleza kuwa hafahamu kama watoto hao watarudi kuendelea na masomo yao kwa kuwa muda wa kufunguliwa shule hizo, umekaribia baada ya likizo ya mwaka kumalizika.

Aliongeza kuwa familia hiyo, iliondoka katika nyumba hiyo na kuacha kila kitu ikiwamo baadhi ya mifugo yao ya kuku na kwa sasa yeye ndiye anayeangalia usalama wa nyumba hiyo kwa kupitia pitia akishirikina na majirani wa kitongoji hicho.

Mwenyekiti wa kitongoji hicho ambaye alijeruhiwa kichwani na sime katika tukio hilo, Mathayo Luoga, alithibitisha familia ya Mtitu kuyakimbia makazi yao kutokana na vitisho vya baadhi ya wafugaji wanaopita nyakati za usiku wakiwa na tochi na kumulika nyumba hadi nyumba.

"Mimi nimetoka hospitali Desemba 27, mwaka huu nimefika hapa na kupewa taarifa na wananchi kuwa familia ya Mtitu imeondoka na kuelekea kusikojulikana ikihofia maisha yao kutokana na vitisho vya baadhi ya wafugaji wanaopita katika kitongoji chetu nyakati za usiku. Suala hili nimelifikisha kwa Mwenyekiti wa Kijiji hiki cha Dodoma Isanga,” alisema.

Alisema kuwa pamoja na familia hiyo kuondoka, lakini zipo familia nyingine katika kitongoji hicho ambazo pia zimeamua kuondoka na kwenda kutafuta hifadhi katika vijiji vya jirani kikiwamo Kijiji cha Nyari kilichopo Kata ya Zombo Tarafa ya Ulaya.

Mmoja wa majirani wa familia hiyo, Alexona Joakim, alisema mke wa Mtitu alimuaga kuwa anaondoka na watoto wake kutokana na tishio la baadhi ya wafugaji kupita nyakati za usiku na kutishia usalama wao.

DOWNLOAD APP YETU YA SWAHIBA NEWS ILI UWEZE KUPATA HABARI ZOTE MOJA KWA MOJA KUPITIA SIMU YAKO YA MKONONI BILA KUINGIA KWENYE WEBSITE,KUDOWNLOAD BONYEZA HAPA  

ANDIKA MAONI YAKO HAPO CHINI
ads
Bonyeza HAPA kudownload applicationi ya SWAHILI NEWS kwenye simu yako ili kupata habari zetu Haraka
Share To:

SWAHIBA MEDIA STAFF

Habari , karibu katika mtandao wetu ili kuhabarika na stori zote za siku katika lugha yetu adhwim ya kiswahili, habarika wakati wote weka dunia kiganjani mwako na swahili news

Post A Comment: