TIMU ya soka ya Tanzania Bara maarufu Kilimanjaro Stars itaanza kampeni ya kuwania ubingwa wa mashindano ya Kombe la Chalenji kwa kuivaa Libya katika mechi ya Kundi A itakayofanyika Desemba 3 mwaka huu jijini Nairobi, Kenya.
Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa jana na Baraza la Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati (CECAFA), Kilimanjaro Stars imepangwa katika Kundi A ikiwa pamoja na wageni Libya, Rwanda, Zanzibar na wenyeji Kenya wakati Kundi B linaundwa na Uganda, Zimbabwe, Burundi, Ethiopia na Sudan Kusini.
Taarifa hiyo iliyotolewa na Katibu Mkuu wa CECAFA, Nicholas Musonye, imesema kuwa Kilimanjaro Stars itashuka tena dimbani Desemba 7 kuwakabili ndugu zao Zanzibar halafu Desemba 9 itakutana na Rwanda na itamaliza mechi zake za hatua ya makundi ifikapo Desemba 11 kwa kuvaana na Kenya.
Musonye alisema kuwa kila kundi litatoa timu mbili zitakazotinga hatua ya nusu fainali ambayo itachezwa kati ya Desemba 14 na 15 mwaka huu huku fainali za michuano hiyo zikitarajiwa kufanyika Desemba 17 kwa kutanguliwa na mchezo wa kusaka mshindi wa tatu wa michuano hiyo ambayo mwaka jana haikufanyika.
Aliongeza kuwa mechi za michuano hiyo zitafanyika kwenye viwanja vitatu tofauti ambavyo ni Kakamega, Nakuru na Kisumu baada ya ule wa Nyayo kuwa kwenye matengenezo.



Post A Comment: