KATIBU wa Bunge, Dk Thomas Kashillilah leo ataeleza kinachoendelea
kuhusu kusudio la Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni kutaka kumwondoa
madarakani Naibu Spika, Dk Tulia Ackson (pichani).
Kambi hiyo inayoongozwa na Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na
Maendeleo (Chadema) Taifa, Freeman Mbowe katika migomo yake dhidi ya
vikao vinavyoongozwa na Dk Ackson, iliwasilisha kusudio hilo kwa Ofisi
ya Spika wa Bunge wiki iliyopita kwa maelezo kuwa haina imani naye.
Kwa mujibu wa Dk Kashillilah, ataeleza kinachoendelea leo baada ya
kumaliza kupitia taratibu zote na kujiridhisha kuhusu kila hatua
inayopaswa kufuatwa kuhusu suala la aina hiyo. “Nitaeleza kinachoendelea
kesho (leo) baada ya kujiridhisha kuhusu taratibu zinazopaswa kufuatwa
kuhusu suala hilo,” alisema.
Katika kusudio hilo lililowasilishwa na Mbunge wa Simanjiro, James
ole Millya, Kambi hiyo ya Upinzani ilieleza mambo sita yaliyoisukuma
kuona kuwa Dk Tulia hafai kuendelea kushika kiti cha Naibu Spika.
Mambo hayo ni upendeleo kwa wabunge wa CCM, kusimamia maslahi ya
Serikali badala ya umma, kutokuwa mwanasiasa, jambo linalomfanya akose
uzoefu wa kuendesha vikao vya Bunge, ubabe, unyanyasaji kwa wabunge wa
upinzani na kusimamia fedha za Mfuko wa Bunge zirudishwe kwa Rais.
Millya alisema walipeleka kusudio hilo kwa Ofisi ya Spika kwa
kuzingatia ibara ya 85(4) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
inayozungumzia hatua za kuchukua ili kumwondoa madarakani Naibu Spika.
DOWNLOAD
APP YETU YA SWAHIBA NEWS ILI UWEZE KUPATA HABARI ZOTE MOJA KWA MOJA
KUPITIA SIMU YAKO YA MKONONI BILA KUINGIA KWENYE WEBSITE,KUDOWNLOAD
BONYEZA HAPA
ANDIKA MAONI YAKO HAPO CHINI
Post A Comment: