WAZIRI wa zamani wa Nishati na Madini na Mbunge wa Jimbo la Sengerema, William Ngeleja amerejesha rasmi Serikalini Shilingi Milioni 40.4 alizopokea kutoka kwa James Rugemalila ambao ni mgao wa kashfa ya Tegeta Escrow.
Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam, Ngeleja amesema 'Nimeamua kurejesha fedha hizi hata kama aliyenipa msaada bado ni mtuhumiwa tu, kwa sababu sitaki kuwa sehemu ya kashfa/tuhuma hizo, '' alisema Ngeleja.
Alisema kuwa ana miaka zaidi ya miaka 12 akiwa kiongozi wa uuma lakini hajawahi kukumbwa na kashfa ya rushwa au ufisadi, hivyo kwa kuwa imedhihirika kwamba aliyempa msaada huo anatuhumiwa kwenye kashfa ya akaunti ya ESCROW amefanya maamuzi ya kurudisha fedha hizo.
"Kupokea msaada ni jambo la kawaida, ila ikibainika kuna harufu ya uchafu hata kama haujathibitishwa na vyombo husika ni vyema kujiepusha nao.....Nimerudisha fedha hizi ili kulinda maslahi ya nchi yangu na heshima ya chama changu, Serikali, wanasengerema, familia yangu na heshima yangu,"alisema Ngeleja.





Post A Comment: