ads

MBUNGE wa Jimbo la Babati Mjini, Pauline Gekul (Chadema), ameibuka na kudai hakutekwa siku ya uchaguzi mdogo wa madiwani Novemba 26, mwaka huu, kama ilivyodaiwa na watu wengi.


Alisema, siku hiyo alikamatwa na polisi pamoja na mawakala aliokuwa nao.

Akizungumza na gazeti la  Nipashe  jana mjini hapa alisema, hakutekwa kama wananchi wengine walivyokuwa wanadai mitaani na katika mitandao ya kijamii, bali alichukuliwa na polisi  kwenda  kituo cha polisi Usa River.

Alisema hatua hiyo ilitokana na wao kuhoji kwa nini mawakala wa Chadema wametolewa nje ya vituo vya kupigia kura.

Alisema alikuwa msimamizi wa kata ya Leguruki iliyopo Arumeru  ambayo ilikuwa inafanya uchaguzi wa diwani  lakini akadai kilichofanyika kilikuwa ni dhuluma na siyo uchaguzi wa kidemokrasia.

“Kwa kweli kwa yale yaliyofanyika Arumeru hakuna  demokrasia tena  nchini, kwa hali ya kawada  na ikibidi mheshimiwa Rais alete  tu mswaada bungeni   kufuta  mfumo wa vyama vingi uliopo,’’ alisema.

“Mfano mtu wa kwanza alipokuwa anaingia kituo cha kupigia kura kama pale Leguruki alikuta sanduku la kura  zimeishafika nusu  na alipouliza aliambiwa toka nje  wakati alikuwa hajawekewa hata mhuri  kiganjani,’’ alieleza.

Aidha,  alisema kitu kilichowatia hofu wananchi kuwa amevamiwa mbunge huyo ni kuona anachukuliwa na polisi pamoja na mawakala wa Chadema.

Alisema iliwachukua muda mrefu kufika kituoni hapo kwa kuwa mmoja wa mawakala aliyekamatwa nao alipata mshutuko na kuanza kutapika na hivyo walianza kumpeleka kituo cha afya ili apate matibabu.

Alisema kilichofanyika  Arumeru  ni ubakaji wa demokrasia  na kwa kuwa mawakala walipewa barua kutoka Tume ya Taifa ya Uchaguzi na wakaapishwa na watendaji wa kata  lakini mkurugenzi alikuja kuwageuka na kuamua kuwabadilisha vituo majira ya saa sita mchana  huku kura zikiendelea kupigwa.

Alisema wananchi waliposikia wamekamatwa waliacha kwenda kupiga kura hivyo kati ya watu 4,000 waliojiandikisha kupiga kura waliopiga kura  ni kama 1,000.

“Sisi tulipokamatwa tuliteswa na maaskari kwa kutumwagia maji ya kuwasha machoni kuanzia mchana hadi usiku matokeo yalipotangazwa mpaka sasa macho yangu hayaoni vizuri,” alisema.

Akizungumzia wimbi la wabunge wa upinzani kuhamia CCM, alisema wanaofanya hivyo hawana msimamo na hawajielewi bali wanaangalia maslahi yao binafsi na ndio maana wanawasaliti wananchi waliowachagua.

Alisema wabunge wa namna hiyo hawafai kuwa wanasiasa kwa sababu hawajui wanachokifanya na wanaposema wanamuunga mkono Rais  ni unafiki  mtupu siyo kwamba inatoka moyoni mwao hali hiyo.

“Watanzania siyo wa kweli  kwa mioyo yao hao wanaoamua kwenda  huko kuacha vyama vyao  hasa wabunge  siyo wanaipenda  CCM bali wana hofu  na ndio maana wanaamua kumuunga mkono adui  lakini wengi wao  wana njaa,’’ alisisitiza.

Alisema wabunge wanaoamua kutimukia CCM ni wale waliokuwa  wanatumiwa na chama hicho.

Alisikitishwa na wabunge vigeugeu  ambao alisema hawaelewi  kwa  kuwa wanafiki kwa kudai wanamuunga mkono Rais wakati  wanaona hali ya uchumi ni mbaya huku akidai wametoka kuambiwa  kwenye vikao kuwa fedha iliyopo kwenye mzunguko ni Sh. bilioni 12 kutoka  Sh. bilioni 200.

Hata hivyo, alishauri  wabunge  wa namna hiyo kuombewa  kwa kuwa hawajui wanachokifanya na akasema watamuungaje mkono Rais wakati wanaona  fedha nyingine inayotumiwa na serikali inakuwa haijatengwa na bunge hivyo anaona hakuna sababu ya kumuunga mkono Rais.  
ads
Bonyeza HAPA kudownload applicationi ya SWAHILI NEWS kwenye simu yako ili kupata habari zetu Haraka
Share To:

SWAHIBA MEDIA STAFF

Habari , karibu katika mtandao wetu ili kuhabarika na stori zote za siku katika lugha yetu adhwim ya kiswahili, habarika wakati wote weka dunia kiganjani mwako na swahili news

Post A Comment: