ads

MBUNGE wa Kigoma Mjini (ACT- Wazalendo), Zitto Kabwe, ametoa utetezi wake kwa hoja 10 mbele ya Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge, akijibu tuhuma zinazomkabili za kulidhalilisha Bunge katika mitandao ya kijamii.



Zitto alikamatwa na Jeshi la Polisi juzi katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Nyerere (JNIA), akitokea mkoani Kigoma na kupelekwa Dodoma mbele ya kamati hiyo kujibu tuhuma hizo.

Katika taarifa aliyoitoa jana kwa vyombo vya habari baada ya kuhojiwa na kamati hiyo, Zitto alieleza alivyojibu tuhuma zinazomkabili kwa kukiri na kutoa utetezi wake kwa hoja zipatazo 10.

“Leo nimefika mbele yenu na nitajibu wito wenu kama ifuatavyo, kwamba maoni yangu kwenye mtandao wa Twitter kuwa "Bunge siku hizi ni idara ya Tawi la Utawala" yanadhalilisha mhimili wa Bunge”.

“Maneno hayo ni yangu na nimeyatoa kama raia wa Tanzania. Ninaamini kwa dhati kuwa Bunge la 11 limekuwa likifanya kazi kwa kuingiliwa na serikali chini ya Rais John Pombe Magufuli,” alisema Zitto.

Hoja 10 za utetezi

Hoja ya kwanza aliyoitoa Zitto alieleza kuwa hatua ya kuzuiwa kwa matangazo ya bunge kwa  kisingizio  cha  kupunguza  gharama  za uendeshaji  wa  mhimili  wa  Bunge,  ni dalili ya wazi ya kufifisha sauti ya Bunge na kupandisha sauti ya serikali.

Hoja ya pili Zitto aliitaja kuwa ni kitendo  cha  uongozi  wa  Bunge  kurudisha  serikalini  Sh. bilioni sita bila ridhaa ya wabunge kwa kisingizio kwamba zimebaki kutokana na kubana matumizi.

Hoja ya tatu ya utetezi huo ni maelekezo ya mhimili wa dola kwa Bunge, kupitia maagizo ya Rais John Magufuli kwa Spika Job
Ndugai kuwa "Awashughulikie wabunge aliowaita "waropokaji", ili waje wazungumze nje ya Bunge na yeye Rais (Serikali) apate nafasi ya kuwashughulikia.

Hoja nyingine ni kitendo cha Bunge kuhariri hotuba za kambi ya upinzani kwa kushinikiza kuondolewa kwa vipengele vinavyoikosoa serikali.

“Mathalani, wakati wa Bunge la Bajeti, hotuba ya Msemaji wa Kambi ya Upinzani wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Godbless Lema, iliamriwa kuondolewa maneno yanayohusu kashfa ya Mkataba wa Lugumi, kumhusisha Rais na kuuzwa kwa nyumba za serikali, mauaji ya wanasiasa, pamoja na Bunge kulinda wahalifu,” alisema Zitto.

Hoja ya tano ni aliyoitoa ni kauli ya Rais Magufuli aliyoitoa Novemba 4, mwaka jana akizungumza na wahariri wa vyombo vya habari kuwa "mzizi wa mhimili wa serikali ni mrefu zaidi kuliko mihimili mingine"  baada ya kuulizwa juu ya matumizi ya serikali nje ya  bajeti  iliyoidhinishwa  na  bunge.

Hoja nyingine ni kitendo cha Ripoti ya Kamati ya Bunge ya Tanzanite na Almasi kusomwa nje ya Bunge na kuwasilishwa kwa Waziri Mkuu na Rais bila kuwasilishwa na  kujadiliwa  Bungeni , ili  kuwekewa  azimio  la  Bunge. 

Zitto alisema kitendo hicho kinaifanya kamati hiyo kuonekana kuwa ya serikali badala ya Kamati ya Bunge.

Hoja ya saba ni kauli  ya  Rais Magufuli  kuwa  Spika  kumpigia simu  kumuuliza  juu  ya wajumbe  wa kuwaweka kwenye Kamati za Bunge za Tanzanite na Almasi.

Hoja nyingine ni kitendo cha Tundu Lissu kushambuliwa kwa risasi wakati Bunge likiendelea, wabunge kukamatwa ovyo ni dharau ya hali ya juu kwa mhimili huo.

Zitto alitaja hoja nyingine kuwa ni kitendo  cha serikali  kutowasilisha  taarifa  za  utendaji  wa  robo  mwaka kwenye  Kamati  ya  Bunge  ya  Bajeti  kama  inavyotakiwa  kwa  mujibu  wa Sheria ya Bajeti ya mwaka 2014.

 Hoja ya mwisho aliyoitoa Zitto ni  Bajeti  ya  Bunge  kutowekwa  kwenye  Mfuko  wa  Bunge  kwa  mujibu  wa sheria na Spika kutakiwa kuomba vibali vya safari za wabunge kwa mkuu wa  tawi  la  utendaji  (serikali).
ads
Bonyeza HAPA kudownload applicationi ya SWAHILI NEWS kwenye simu yako ili kupata habari zetu Haraka
Share To:

SWAHIBA MEDIA STAFF

Habari , karibu katika mtandao wetu ili kuhabarika na stori zote za siku katika lugha yetu adhwim ya kiswahili, habarika wakati wote weka dunia kiganjani mwako na swahili news

Post A Comment: