ads
Azam FC jana imefanikiwa kuingia kwenye fainali ya mashindano ya Kagame Cup baada ya kuiondosha timu KCCA ya Uganda kwa goli 1-0 kwenye mchezo wa nusu fainali uliopigwa jana jioni katika uwanja wa Taifa.
Azam wameweka rekodi ya kuwa timu iliyotinga hatua ya fainali ya michuano ya Kagame mwaka 2015 ikiwa haijaruhusu goli ndani ya dakika 90 huku ikiwa imefunga jumla ya magoli 10 kuanzia hatua ya makundi hadi mchezo wa nusu fainali.
Kutofungwa goli hata moja inadhihirisha kuwa safu ya ulinzi ya Azam ni bora zaidi ambayo imekuwa haipenyeki kirahisi na washambuliaji wa timu pinzani pindi wanapokutana. Ukuta wa Azam ukiongozwa na Pascal Wawa umekuwa imara na hiyo imepelekea beki huyo (Wawa) kutangazwa kama mchezaji bora wa mechi (man of the match) mara mbili wakati Manula yeye akiwa amechukua mara moja.
Kesho Azam inakutana na Gor Mahia ya Kenya kwenye mchezo wa fainali ambao unatabiriwa kuwa ni mchezo mgumu na wa upinzani mkubwa. Ugumu wa mchezo huo unasababishwa na aina ya wachezaji wanaokutana kwenye mchezo wenyewe.
Kwa upande wa Gor Mahia, wao silaha yao kubwa imekuwa ni mshambuliaji wao Michael Olunga ambaye ndiye anaeongoza kwa magoli hadi sasa akiwa ameshatupia wavuni jumla ya magoli matano. Olunga ni aina ya mshambuliaji amabae anajua vizuri kutumia nafasi zinazotengenezwa, anapopata nafasi basi anakuwa ni mtu hatari sana kutokana na uwezo wake mkubwa wa kuzifumania nyavu.
Kagere Medie, Godfrey Walusimbi na Haruna Shakava ni wachezaji wengine ambao ni moto wa kuotea mbali kwa upande wa Gor Mahia na wanahitaji uangalizi wa haili ya juu pindi wawapo uwanjani kwani wanauwezo mkubwa wa kufanya lolote litakalo badili matokeo wakati wowote wa mchezo.
Azam wao pia wanawachezaji ambao ni nguzo ya timu yao na mara nyingi wanaonekana kuibeba timu iwapo uwanjani. Uwepo wa Pascal Wawa kwenye safu ya ulinzi unaifanya Azam kutokuwa na presha kubwa kwani Wawa ni mchezaji anaeyatambua vyema majukumu yake. Kipre Tchetche licha ya kuwa anapoteza nafasi nyingi za kufunga lakini bado ni mchezaji wa kuogopwa hasa kwenye mchezo wa fainali.
Farid Mussa ni mlinzi wa kushoto wa Azam na amekuwa kwenye kiwango bora sana tangu kuanza kwa michuano hii, anaweza kukaba vizuri na kupandisha mashambulizi pale timu yake inapokuwa inashambulia. Jana alifunga goli pekee lililoivusha Azam na kuipeleka kwenye hatua ya fainali ya Kagame, ni mchezaji mwingine wa kuangaliwa sana na timu ya Gor Mahia.
Mugiraneza licha ya kujiunga na Azam siku za hivi karibuni ameonekana ni mchezaji ambaye anakipaji cha hali ya juu hasa anapocheza katika eneo la kiungo wa ulinzi, aweza kukaba vizuri, anacheza mipira ya juu lakini pia anauwezo wa kupiga pasi ndefu.
Azam imeingia hatua ya fainali kwa mbinde kutokana na kupata upinzani wa hali ya juu kutoka kwa KCCA tofauti na wengi walivyokuwa wanatarajia. Gor Mahia wao wametinga hatua hiyo kwa ushindi wa goli 3-1 walioupata kutoka kwa timu ngumu na ngeni kwenye mashindano haya Khartoum ya Sudani.
Kesho kutakuwa na mechi ya kumpata mshindi wa tatu itakayo zikutanisha timu zilizofungwa jana kwenye nusu fainali ambazo ni KCCA dhidi ya Khartoum mchezo utakaotangulia mchana kabla ya fainali ya mashindano hayo kupigwa kati ya Azam FC dhidi ya Gor Mahia.
ads
Bonyeza HAPA kudownload applicationi ya SWAHILI NEWS kwenye simu yako ili kupata habari zetu Haraka
Share To:

SWAHIBA MEDIA STAFF

Habari , karibu katika mtandao wetu ili kuhabarika na stori zote za siku katika lugha yetu adhwim ya kiswahili, habarika wakati wote weka dunia kiganjani mwako na swahili news

Post A Comment: